Friday, April 20, 2012

Lulu hakumbukwi na wasanii wenzake

KITENDO cha mastaa wa filamu kushindwa kwenda kumtembelea msanii mwenzao, Elizabeth Michael ‘Lulu’, anayekabiliwa na kesi inayohusisha kifo cha aliyekuwa mwigizaji, Steven Kanumba, katika gereza la Segerea jijini Dar ni kukwepa kuhusishwa katika keshi hiyo, imefahamika.
Uchunguzi uliofanywa umebaini kuwa kumekuwa na mahudhurio hafifu ya wasanii maarufu kwenda kumtembelea Lulu katika gereza hilo.


Akielezea hali hiyo, kiongozi mmoja wa Bongo Movie, alisema ni kweli hali hiyo ipo na wengi wanaogopa kuhusishwa katika kesi hiyo kwa kuwa bado uchunguzi wake unaendelea.
“Napingana na hoja ya kusema sisi mastaa ni wanafiki, binafsi ninachokiogopa mimi na wenzangu ni majumba mabovu ambayo yanaendelea kubomoka (kuingizwa kwenye tuhuma) kila siku kuhusiana na kesi ya Lulu, ndiyo maana wengi wanaogopa kwenda Segerea,” alisema kiongozi huyo.
Lulu ambaye anatuhumiwa kuhusika na kifo cha Kanumba, ameshapandishwa kizimbani mara moja na atarejea tena Aprili 23, mwaka huu.


Kanumba alifariki dunia usiku wa kuamkia Aprili 7, mwaka huu, nyumbani kwake Sinza Vatican, Dar na kuzikwa Aprili 10 katika makaburi ya Kinondoni.

Jamani sajuki anaumwa.


UKWELI ni kwamba, staa mkubwa wa filamu za Kibongo, Sadick Juma Kilowoko ‘Sajuki’ anaumwa.
Hali ya Sajuki imeendelea kuwa mbaya akidhoofu mwili siku hadi siku kutokana na kusumbuliwa na tatizo la uvimbe tumboni kwa muda mrefu sasa.


Aprili 15, mwaka huu Sajuki na mkewe Wastara Juma walifanya sherehe ya 40 ya kumtoa mtoto wao, Farheen ambayo ilihudhuriwa na waandishi wetu waliomshuhudia msanii huyo akiwa amedhoofu sana.Kabla ya kuugua, Sajuki alikuwa mwanaume aliyeshiba (mnene) na mwenye nguvu hivyo kutokana na hali yake ilivyobadilika na mwili kuwa mdogo, baadhi ya wasanii waliofika kwenye sherehe hiyo walijikuta wakimtolea machozi.
“Jamani tuacheni utani, Sajuki anaumwa sana na anahitaji msaada na maombi yetu ili arejee kwenye hali yake ya kawaida,” alisema mmoja wa waigizaji wenzake.


Kwa mujibu wa mkewe Wastara, Sajuki alipokwenda katika Hospitali ya Apollo nchini India hivi karibuni alipewa dawa za kutumia kwa muda ambapo mwezi ujao (Mei) alitakiwa kurejea tena nchini humo kwa ajili ya matibabu zaidi.

WADAU TUMSAIDIENI SAJUKI
Kufuatia hali ilivyo, blog hii inaomba wadau tujitokeze kumchangia Sajuki fedha kwa ajili ya matibabu kupitia simu ya mkononi kwa kutuma kwenye Tigo Pesa namba 0713 666 113 au kwenye akaunti namba 050000003047 katika Benki ya Akiba Commercial yenye jina la Wastara Juma Issa.


Aibuka Mwingine tena.........soma habari zaidi


SALMA Hamidu, mkazi wa Igogo, jijini Mwanza ameibuka na kudai amezaa na marehemu Steven Kanumba mtoto wa kike aitwaye Treasure Steven Charles Kanumba (2), Ijumaa linashuka na maneno ya kinywa chake.
Akizungumza na mwandishi wetu, Salma anayefanya kazi kwenye Ofisi ya Uwakili ya Law Consultancy jijini Mwanza, alidai alianza kufahamiana na marehemu mwaka 2006 wakati yeye akiwa kwenye Kundi la Nyakato Arts chini ya Mwalimu Joseph.
CHANZO CHA UHUSIANO
Salma akasema kuwa, uhusiano wao uliunganishwa na Mwalimu Joseph ambaye alimpa marehemu namba zake za simu wakati alipopeleka filamu za Machozi Yangu na Siri Yangu kuifanyia uhariri (editing) jijini Dar es Salaam katika studio alizokuwa akifanyia kazi marehemu.
“Marehemu alipoona picha zangu kwenye filamu hizo alivutiwa na mimi katika kuigiza, akaomba namba zangu za simu kwa Mwalimu Joseph,” alisema Salma.
Mrembo huyo aliendelea kuweka wazi kuwa, baadaye Mwalimu Joseph alirejea Mwanza na kumtaka radhi kwa kumwambia alimpa Kanumba namba zake za simu.



LAIVU KWA MARA YA KWANZA
“Mwaka 2007, Kanumba aliniita Dar, alinitumia tiketi ya ndege ya Precision Air, kwetu niliaga nakwenda kumsalimia mama mkubwa anayeishi Tabata.
“Nilipofika Dar, nilimpigia simu Kanumba kumtaarifu nimefika, akanitaka tukutane Ubungo Plaza Hotel (Blue Pearl),” alisema Salma.
Pale Ubungo Plaza, marehemu kwa mara ya kwanza alimtamkia lililo moyoni mwake kwamba ametokea kumpenda na akamuomba wawe wapenzi.
“Sikuwa na uamuzi wa haraka, lakini kutokana na ushawishi wake nilikubali, baadaye nilirudi Tabata kwa mama mkubwa.
“Usiku alinipigia simu, akaniomba kesho yake tusafiri kwenda Zanzibar, nilikubali, asubuhi niliaga kwa shangaza tukaenda Zanzibar.
“Tulifikia Bwawani Hoteli. Tulikaa kwa siku tatu na kwa mara ya kwanza nilikutana na marehemu kimwili. Tuliporudi Dar mimi nikarejea Mwanza,” alisema Salma.
KANUMBA PENZI LAKOLEA, ATUA MWANZA
“Baada ya kama miezi minne na siku kadhaa hivi, marehemu alinipigia simu akasema yuko Mwanza, anataka kuja chuoni kuniona. Alikuja akiwa ameongozana na marafiki zake wawili, Credo na Theonist Rutashoborwa.
“Walikuja hadi chuoni, mimi nilitoka tukaenda kukaa kwenye baa ya Shentemba. Ilipofika saa 2 usiku, tukahamia Isamo Hotel,” alisema Salma.
Salma aliendelea kusema kuwa, pale Isamo walipata chakula kabla ya kujitupa kitandani lakini siku hiyo muda mwingi alikuwa akijisikia vibaya, marehemu akamtaka asubuhi akapime.
“Asubuhi nilikwenda kwenye Kliniki ya Dokta Ng’walida, daktari bingwa wa magonjwa ya akina mama na watoto. Vipimo vilionesha nilikuwa na ujauzito wa miezi minne.
“Nilimwonesha marehemu majibu yale, hakuonekana kukubali wala kukataa, lakini baadaye akasema kazi yake haimruhusu kuwa na mtoto wala familia hadi atakaponiambia.
“Baada ya siku mbili, aliaga kurejea Dar pamoja na marafiki zake. Siku chache baadaye huku nyuma kwa bahati mbaya ujauzito ulitoka, nilikwenda kwa daktari mmoja Nyakato National ambaye alithibitisha hilo. Huo ulikuwa mwaka 2008.


UJAUZITO WA PILI
Salma alisema kuwa mawasiliano na marehemu yaliendelea. Kuna siku alimpigia simu akimtaka wakutane jijini Arusha.Alipofika alipokelewa na Kanumba mwenyewe kabla ya kwenda kupiga kambi kwa rafiki yake mmoja aliyekuwa akiishi peke yake.Akasema kukutana kwao kimwili kwa safari hii, ndiko kulimpa ujauzito na hatimaye kujifungua binti anayeitwa Treasure au Tunu.
Arusha waliondoka na ndege hadi Mwanza ambapo walifikia Ladson Hotel, ipo Bwiru na kukaa kwa siku mbili kabla ya kumruhusu kurejea nyumbani kwao Igoma. Akiwa na ujauzito huo, Kanumba alimtumia nauli akimtaka wakutane mjini Morogoro.“Nikiwa na tumbo langu, aliniita Morogoro, nilisafiri kwa basi hadi kule, nilifikia kwa shangazi yangu yeye alipanga kwenye hoteli ipo jirani na Kituo cha Mabasi cha Msamvu.

KANUMBA ATOA ONYO
“Kulitokea kutokuelewana kidogo na marehemu kwa sababu ya ujauzito ule, akirejea mazungumzo yake ya awali kuwa, kazi yake haimruhusu kuwa na mtoto wala familia, lakini nilimwambia sina namna ya kufanya kuhusu ujauzito ule.“Hata hivyo, marehemu alinionya nisimwambie mtu kuhusu ujauzito kuwa ni wa kwake, iwe siri yangu na yake kwa sababu hakutaka habari hiyo ifike kwenye magazeti,”alisema Salma.Akaongeza: Baada ya hapo, alinipa shilingi 150,000 nikarudi nyumbani Mwanza.“Nikiwa Mwanza alikuwa akinipigia simu akitaka kujua naendeleaje na tumbo langu na kunitaka nijiandae kwa safari ya Dar, atanitumia tiketi ya ndege. “Nilisafiri, nilipofika Dar nilimjulisha, akasema tusikae Dar, twende Zanzibar. Kule tulifikia tena Bwawani Hotel. Tulikaa kwa siku nne, kisha tukarejea Dar.

Lakini tukiwa Zanzibar kuna mtu alinipigia simu na yeye akiwepo, alikasirika sana na kuninyang’anya simu, akachukua namba kisha akampigia mtu huyo, waligombana kwenye simu. Aliipasua simu yangu, akaenda kuninunulia nyingine.“Alikuwa mtu mwenye hasira, hakutaka kusikia unazungumza na simu hasa ikiwa ni sauti ya kiume. Ugomvi huo ulisababisha aikane mimba, akasema namsingizia ni ya mwanaume aliyenipigia simu. Ilifika mahali akasema kila mtu aishi kivyake.“Hata hivyo, alikuja kuniomba msamaha huku akizidi kunionya kuwa ole wangu nitangaze nina mimba yake.” Alisema ugomvi wake na Kanumba ulitokana na ujauzito na ilifika mahali Salma alimweleza mama yake ambaye alimlaumu kwa kujiingiza kwenye uhusiano na mwanaume huyo.


MISAADA KUTOKA KWA KANUMBA
Kwa upande wa misaada, Salma alisema akiwa mjamzito, marehemu alimtumia shilingi Milioni  mbili na laki mbili kwa ajili ya kununua kiwanja. Baadaye alimtumia shilingi Milioni moja za kupanga nyumba. Fedha hizo alizituma kupitia Benki ya Standard Chartered Tawi la Mwanza.
Baada ya kutuma fedha hizo, marehemu aliwahi kwenda Mwanza na kufikia kwenye Hoteli ya Ryans Bay. Wakati huo mimba ilikuwa na umri wa miezi saba.

HAKUTAKA KUPIGA NAYE PICHA
Salma anasema: Nilimtaka tupige picha ya ukumbusho akakataa, lakini nilipojifungua alikuja na kumpiga picha mtoto kwa kutumia simu yake akisema, ‘mtoto mama yangu mtupu kwani amefanana naye sana.’ Aliongeza kuwa alipojifungua Kanumba alimtumia shilingi 500,000 za matumizi ya mtoto kupitia simu ya mama yake mzazi na Salma (hakumtaja jina). Aliendelea kusema kulijitokeza sakata wakati wa kumpa jina mtoto, Kanumba akitaka amwite jina la mama yake, huku Salma naye akitaka kumwita la mama yake, ndipo wakakubaliana mtoto aitwe Treasure au Tunu ili kumaliza mzozo wa kugombea kumwita mtoto jina la upande mmoja. “Treasure alipofikisha miezi saba alisema nimpige picha nimtumie ili amwone alivyofikia, nilifanya hivyo. Siku moja akaniambia angetunga filamu kuhusu maisha yetu ambayo alipendekeza iitwe My Gift. “Siku chache kabla ya kifo chake alinipigia simu pamoja na mtoto akisema alitaka kusafiri na asingekuwepo kwa mwezi wote wa Machi mwaka huu, alimsamilia mwanaye. Lakini cha kushangaza siku chache nikapewa taarifa za kifo chake,” alisema Salma.
 
KWA NINI USIRI?
Salma alisema mpaka sasa anashindwa kuelewa ni kwa nini marehemu alitaka uhusiano wao uwe wa siri. Lakini baadhi ya marafiki zake walikuwa wakifahamu uhusiano huo.


NENO LA MWISHO LA SALMA
“Kanumba kaniacha njia panda, sijui la kufanya, lakini ni vyema kama angemtambulisha mwanaye kwa ndugu zake kuliko hivi sasa ambapo mengi yatazuka kuwa pengine natafuta fedha za marehemu.
“Sijaweka wazi ili nipate chochote, bali nahisi dhambi kuficha kwa sababu huyu mtoto si damu yangu peke yangu.“Nitakuwa mbaya kwa Mungu kama nisiposema ukweli. Angekuwepo mwenyewe nisingesema kwa sababu yeye ndiye alikuwa kiongozi wa maisha ya mtoto.
“Narudia tena, nina uwezo wa kumlea na wala sihitaji mtoto achukuliwe na kwenda kuishi kwa baba, ila familia ijue kuna damu yao kwangu.“Kama hawataamini, niko tayari kufika Dar na kupima DNA ili familia ya marehemu ijiridhishe,” alisema Salma.

Hata hivyo, Salma alikiri kufanya kosa la kutowahusisha marafiki wa Kanumba kumtegulia kitendawili hicho na kudai pengine umri mdogo ulichangia. Salma alizaliwa mwaka 1987.
Alisema mtu pekee ambaye watu wanamfahamu na ndiye shahidi wa uhusiano wake na marehemu ni msanii wa maigizo, Ramadhan Malele ‘Swebe’ ambaye alikuwa akiwasiliana naye mara kwa mara.
Salma alisema kabla Kanumba hajafikwa na mauti, yeye aliwahi kukutana na Swebe jijini Mwanza ambapo alimsimulia hali ilivyo na akamshauri kusikiliza matakwa ya marehemu ya kutotoa siri ya kuwepo kwa mtoto huyo.

Monday, April 9, 2012

Rest in Peace our beloved STEVEN CHARLES KANUMBA 1984-2012

STEVEN CHARLES KANUMBA 1984-2012
Daima majonzi yetu yatakuwa pamoja na watazania kwa ujumla juu ya kifo cha mwenzetu mpendwa wetu Steven Kanumba, ambae kwa sisi tulipata bahati ya kumzawadia tuzo ya 'the best male actor 2009' ya Smilingfaces RedCarpet awards.

Marehemu akipokea tuzo yake ya the best male actor 2009 redcarpet awards
 Team nzima ya Smilingfaces Company pamoja na mimi Carolyne Zayumba tunasema tumemkosa mpiganaji wa ukweli ambae nyota yake ama ndoto zake ni kutoa ujuzi wake Hollywood baada ya kuona kwa hapa Africa ameweza gusa nyoyo za watu na kuonyesha uwezo wake na kipaji chake cha uigizaji.
Marehemu Kanumba akiwa na Jack Wolper baada ya kupokea tuzo zao
Sina Mengi ya kusema zaidi ya kumwomba Mungu amlaze mahali pema peponi. Amina.

APRILI 9, 2012 Mazishi ya Kanumba, taarifa


KAMATI YA MAZISHI YA MSANII STEVEN CHARLES KANUMBA
    Taarifa kwa vyombo vya habari
        APRILI 9, 2012


Msanii wa filamu, aliyebeba mapenzi makubwa ya Watanzania, Waafrika na dunia kwa jumla, Steven Charles Kanumba aliyefikwa na mauti ghafla Aprili 7, 2012, atazikwa kesho Makaburi ya Kinondoni, Wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam.
Mazishi ya Kanumba, yamepangwa na kuratibiwa kwa kuzingatia heshima, umaarufu, mapenzi yake kwa watu na hadhi ya kimataifa aliyonayo, hivyo imetolewa fursa ya wengi kumuaga msanii huyo ambaye ni mwanamapinduzi wa tasnia ya filamu ukanda wote wa Afrika Mashariki na Kati.
Mpangilio wa ratiba na nafasi itatolewa kwa kila mtu mwenye kuhitaji kushiriki mazishi ya Kanumba, kufanya hivyo katika tukio la kihistoria la kumsindikiza ndugu yetu huyo kwenye maisha ya milele. Hivyo, wito unatolewa kwa kila mtu kujitokeza kwenye shughuli nzima.
RATIBA
Mwili wa marehemu Steven Kanumba utachukuliwa kwa msafara kutoka Hospitali ya Taifa, Muhimbili saa 2:30 asubuhi. Utapitishwa Barabara ya Umoja wa Mataifa na Ali Hassan Mwinyi hadi Viwanja vya Leaders Club, Kinondoni ambako Misa ya kumuombea itasomwa pamoja na salamu mbalimbali kabla ya watu wote kumuaga.
Wito unatolewa kwa watu kujitokeza kwa wingi kuanzia saa 2:00 asubuhi, wakijipanga kando ya Barabara za Umoja wa Mataifa na Ali Hassan Mwinyi ili wautolee heshima mwili wa Kanumba wakati ukitolewa Muhimbili kwenda Leaders Club.
Saa 3:30 asubuhi, mwili wa Kanumba utapokelewa Viwanja vya Leaders, ukitanguliwa na mapokezi ya wazazi wake, viongozi mbalimbali wa serikali ambao juu yao kabisa atakuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Mohamed Gharib Bilal.
Saa 4:00, itakuwa ni muda wa kusoma Misa ambayo itachukua dakika 60, saa 5:00 kitakuwa kipindi cha salamu kutoka kwa watu mbalimbali.
Saa 6:00 mchana, ratiba ya kumuaga Kanumba itaanza mpaka saa 9:00 alasiri na baada ya hapo, utakuwa wakati wa kuusafirisha mwili kwa msafara kutoka Leaders Club mpaka Makaburi ya Kinondoni, msafara ukipita Barabara ya Tunisia, utakatisha Barabara ya Kinondoni kuelekea makaburini.
Saa 10:00 alasiri, mazishi yatafanyika kwa kufuata utaratibu wa imani ya marehemu.
Kamati ya Mazishi inatoa wito kwa watu watakaohudhuria shughuli ya kumzika ndugu yetu Kanumba, kuja na maua ili kumuaga kwa heshima.
Utulivu, unyenyekevu na ustahimilivu ni mambo muhimu yanayohitajika katika kipindi chote cha kumuaga mpendwa wetu Kanumba.
Bwana alitoa, Bwana ametwaa. Sisi wote tulimpenda kwa dhati na tulitamani aendelee kuwa nasi siku zote ila Mungu aliyemleta kwa mapenzi yake ameamua kumchukua. Jina lake lihimidiwe.
                                            K.N.Y GABRIEL MTITU
                                   MWENYEKITI WA KAMATI YA MAZISHI

MAJONZI SIMANZI KATIKA MSIBA WA MPENDWA WETU STEVEN KANUMBA R.I.P

 NYOTA ya msanii maarufu wa sinema za Tanzania, Steven Charles Kusekwa Kanumba imezimika ghafla kufuatia kuanguka chumbani kwake na kufariki dunia katika tukio linalohusishwa na ugomvi baina yake na msanii mwenzake, Elizabeth Michael ‘Lulu’ na hii ndiyo ripoti kamili.
CHANZO
Tukio hilo la kusikitisha na lililoacha machozi nyuma yake, lilijiri usiku wa Aprili 7, mwaka huu maeneo ya Vatican City Hotel, Sinza Kijiweni, jijini Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa mdogo wa marehemu aitwaye Sethi Bosco, staa huyo alikuwa chumbani kwake na Lulu, baadaye alisikia kelele za mzozo kutokea huko.
Akasema, kilichofuata baada ya mzozo huo, Lulu aliondoka ghafla, yeye akaenda chumbani na kumkuta Kanumba yuko chini, bila kujua kilichomsibu.
Kijana huyo ambaye alikiri kwamba Kanumba alikuwa amekunywa pombe usiku huo, aliendelea kusema:
“Nilipofika chumbani nilimkuta (Kanumba) amekaa chini huku ameegemea ukuta. Baada ya kumchunguza nikaona anatokwa na povu na damu kinywani.
“Niliampigia simu daktari wake na kumweleza hali hiyo, naye alifika haraka na kuanza kumfanyia uchunguzi.”
AKIMBIZWA MUHIMBILI
Sethi alisema daktari alipomchunguza alishauri akimbizwe Muhimbili. “Tulipofika alifanyiwa uchunguzi na kugundulika kuwa, alishafariki dunia muda mrefu,” alisema kwa uchungu kijana huyo.

MASTAA WAFURIKA MUHIMBILI
Habari zaidi zinasema kuwa, katika hali isiyotegemewa, mastaa mbalimbali, wakiwemo wa sinema, wacheza mpira na wanamuziki, walianza kumiminika katika hospitali hiyo ya taifa ili kujiridhisha na habari za kifo cha Kanumba.
Wengi wakiwa bado hawaamini, walipofika na kuhakikishiwa waliangua vilio, wengine kupoteza fahamu na kupewa huduma ya kwanza.

 ASKARI WACHARUKA
Saa 10 alfajiri huku mastaa wakizidi kuwasili, askari wa Muhimbili walilazimika kuwaondoa waombolezaji hao kwa madai kuwa vilio vyao vilikuwa vikivuruga utaratibu mwingine wa hospitali hiyo.
Ndipo Mwenyekiti wa Bongo Movie Club, Jacob Steven ‘JB’ alipoanza kutumia nguvu ya ziada kuwataka wasanii hao kuondoka eneo hilo na kwenda nyumbani kwa marehemu kwa ajili ya maombolezo na taratibu nyingine.
Hata hivyo, mpaka saa nne asubuhi bado kulikuwa na wasanii wengine wa filamu katika hospitali ya Muhimbili wakiwa hawaamini kifo cha mwenzao.

ALIKUWA NA MIPANGO YA KWENDA MAREKANI
Kwa upande wake, mama mzazi wa marehemu akiongea tokea Bukoba alikokwenda, alisema mwanaye huyo alimpigia simu hivi karibuni na kumuomba arudi Dar ili waagane kwa vile alikuwa kwenye mipango ya kwenda Marekani.
 KWA NINI LULU?
Msanii wa filamu, Lulu alidakwa na maafande wa Kituo cha Polisi cha Oysterbay jijini Dar akidaiwa kuisadia polisi kufuatia kifo cha Kanumba.
Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, Charles Kenyela alisema Lulu alikamatwa kwa sababu ni mshukiwa wa kwanza wa kifo hicho kwa vile alikuwa mtu wa mwisho kuwa na marehemu usiku wa tukio.

JE, NI KWELI WALIKUWA WAPENZI KITAMBO?
Madai yaliyotua juu ya meza ya gazeti hili yanasema kuwa, Lulu na Kanumba wamekuwa wapenzi kwa muda mrefu huku wakikutana kwa siri, hali iliyozua maswali kutoka kwa watu waliokuwepo msibani hapo.
“Jamani, kwani ni kweli Lulu alikuwa mpenzi wa Kanumba? Mbona haiwezekani? Kama  ni kweli basi walikuwa na siri kubwa,” alisikika akisema mwombolezaji mmoja.
Mama mwenye nyumba wa marehemu Kanumba (jina lake halikupatikana mara moja) alisema ameshamuona Lulu mara kadhaa akiwa na Kanumba nyumbani hapo.

KILICHOMUUA CHAJULIKANA
Kwa mujibu wa daktari mmoja wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili ambaye hakuwa tayari kutaja jina lake, kinachoonekana marehemu alijigonga kichwa mahali pagumu, akapata tatizo la kuvuja damu kwa ndani (internal bleeding).
Akasema kwa mtu anayepata tatizo hilo ni rahisi kufariki dunia au akipona anaweza kupatwa na ugonjwa wa kurukwa na akili.
“Kuna uwezekano mkubwa (Kanumba) angepona angeweza kuwa na tatizo la akili,” alisema daktari huyo.


MAISHA YAKE KUELEKEA KIFO
Majirani wa marehemu walisema kuwa, saa mbili usiku wa tukio, Kanumba alitoka nje akionekana mwenye hasira, baadhi ya watu wake wa karibu walimchukua na kumrudisha ndani.
Mpaka tunakwenda mitamboni, habari zinadai marehemu Kanumba anatarajiwa kuzikwa kesho jijini Dar es Salaam.
Mungu ailaze pema peponi, roho ya marehemu Steven Kanumba. Amina.