Thursday, January 26, 2012

JE KUNA UMUHIMU GANI KATIKA KUTAFUTA VAZI LA TAIFA?

Hivi karibuni kumekua na mzozo mkubwa wa kujadili umuhimu wa kuwa na vazi la taifa. Hii ni baada ya waziri wa habari na Michezo Mheshimiwa Emmanuel Nchimbi kutoa siku 75 kwa wadau na wabunifu mbali mbali kujadili kuhusu ili suala la vazi la taifa.

Katika mada hii nimeona mijadala mbali mbali kwenye vyombo vya habari na hata mitaani maana kile kinacho ongelewa habarini ndio hicho hicho hujadiliwa mitaani. Lakini nimeona hii mada ni muhimu sana kuiweka kwenu ili tuone katika ualisia wake umuhimu wa kuwa na vazi hili hususan baada ya kuona kwamba kuna mijadala ambayo inapinga kusiweko na mada hii kwasababu eti inatupotezea muda.

Nikitoa mfano wa makala moja niliyoisoma hivi karibuni kwenye gazeti, nanukuu :  WAKATI nchi ikikabiliwa na matatizo mengi makubwa na mazito, serikali kwa kupitia Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, imezua kwa mara nyingine tena mjadala usiokuwa na tija yoyote kwa wananchi hususani walalahoi – mjadala wa kutafuta vazi la taifa! Mwisho wa kunukuu.

Ya kiwemo mengi yaliyosemwa ambayo mimi sitaweza kuyataya humu kwa kuogopa kukuchosha, ningependa niseme kitu kimoja. Tanzania ni nchi yenye utajiri mkubwa wa maliasili na utamaduni. Sasa nikiwa kama mbunifu wa mitindo na mdau mkubwa wa utamaduni wa kiafrika ninaona si vyema kutumia vazi la kimasai kama kutambulisha Taifa zima la Tanzania. kwanini nasema hivyo? Wamasai ni asilimia ndogo sana ya makabila ya kitanzani na isitoshe wamasai hata kenya wapo. Sasa iweje leo watuongoze kwenye vazi la taifa?

Tukiangalia historia na Picha ninayo hapo juu, Mwalim aliamua kufanya vazi la mgolole lenye asili ya Tabora na Mwanza kuwa vazi la taifa na pia ukiangalia makabila mengi yalikua na asili inayofanana na vazi hilo ila kwa jina tofauti. Mwalim na wenzake kama Sir George Kahama, Rashid Kawawa na wengine wali vaa vazi hilo Kujitambulisha kwamba wao ni Watanganyika na hiyo ndio utambulisho wao (identity) kama taifa hivyo waingereza hawana Budi kutoa uhuru haraka kwa kataifa hili.

Ni kweli Tanzania ya sasa imekumbwa na matatizo mengi ya kiuchumi , kijamii na kisiasa lakini ukweli unabaki pale pale kwamba utambulisho wa taifa ni Muhimu. Hebu tumwone mfalme mswati wa Swaziland, ni mara chache sana anavaa mavazi ya kawaida kama Suti ama mashati na tai, muda mwingi yupo katika mavazi ya kwao ambayo yanampa utambulisho wa kipekee kitaifa na kimataifa.
Mpaka hapo nadhani utakuwa umepata mwangaza wa kwanini taifa hili linaitaji vazi la taifa. Utambulisho ni muhimu pale utakapo kuwa umevaa tofauti na wengine kwa rangi za bendera ya nchi yako ambayo mtu akiona tu atapendezwa nayo ni muhimu sana ndio maana serikali kupitia wizara husika infanya mchakato huo.
Ingawa najiuliza serikali ilikuwa wapi  miaka yote hiyo lakini kwa kufanya uamuzi huo sasa nawapa heko kwa kuona umuhimu wa kumpa Mtanzania utambulisho ambao atajivunia nao. Ningependa nichukue nafasi hii kumpongeza waziri Nchimbi na kamati zima ya vazi la taifa akiwemo Mwenyekiti Joseph Kusaga na Bwana Merinyo kwa kazi nzuri wanayoifanya.




No comments:

Post a Comment

wadau unakaribishiwa kutoa comment ilimradi ziwe za kujenga na kuelimisha pia